Pages

Tuesday, April 9, 2013

Benki ya Posta Tanzania yarekodi faida ya zaidi ya Shilingi bilioni tano


Picture
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Posta Tanzania, Sabasaba Moshingi (kulia) akizungumza na wanahabari leo.
Picture
Mkurugenzi wa Teknolojia na Uendeshaji wa Benki ya Posta Tanzania, Jema Msuya akielezea juu ya usalama wa fedha za wateja wao na huduma ya TPB popote.
Na Mwandishi Wetu

BENKI ya Posta Tanzania (TPB) imepata faida ya jumla ya sh. bilioni 5.6 kabla ya kodi (profity before tax) ikiwa ni faida iliyopatikana kwa mwaka ulioishia Desemba 2012. Taarifa hiyo imetolewa muda mfupi uliopita jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Posta Tanzania, Sabasaba Moshingi, alipokuwa akizungumza na waandishi habari Makao Makuu ya Benki hiyo.

Akifafanua zaidi, Moshingi alisema kiasi hicho cha fedha ni mafanikio makubwa kwa taasisi hiyo ya fedha kwani ni ongezeko la sh. bilioni 1.8 zaidi ukilinganisha na faida iliyopatikana mwaka 2011.

“Faida baada ya kodi kwa mwaka 2012 imefikia shilingi billion 4 Kutoka bilioni 2.5 ya mwaka 2011 sawa na ongezeko la shilling billioni 1.5  Sawa na asilimia 58. Kwa upande wa mapato, benki ilipata mapato ya shillingi billioni 31 ukilinganisha na billioni 24.6 iliyopatikana mwaka 2011…hili ni ongezeko la sh. 5.4 billion sawa na asilimia 22,” alisema Moshingi.

Alisema mbali na faida hiyo benki imeongeza idadi ya wateja kutoka 602,000 hadi kufikia 631,000 ikiwa ni ongezeko la wateja takribani 29,000  sawa na ongezeko la asilimia 5.

“Amana za wateja (Customer Deposits) ziliongezeka hadi kufikia shillingi bilioni 138.8 kutoka shilingi  bilioni 120.9, ongezeko la shilingi bilioni 17.9 sawa na asilimia 15…amana za benki (total assets) ziliongezeka hadi kufikia shilingi bilioni 167.2  kutoka bilioni 136.2 za mwaka 2011 ambalo ni sawa na ongezeko la shilingi bilioni 31 sawa na asilimia 23,” alisema.

Aidha alisema benki hiyo imekopeza kwa wateja wake kiasi cha sh. bilioni 100, kutoka sh. billioni 66 zilizokopeshwa mwaka 2011. Alisema ongezeko hilo ni ni sawa na shillingi billioni 34.

“…Sehemu kubwa ya mikopo hii imetolewa kwa wafanyakazi wa taasisi za umma na serikali pamoja na wafanyabiashara wadogowadogo na wa kati. Faida na mafanikio haya yametokana na imani kubwa waliyotupa wateja wetu kwa kuweka amana kwenye benki yetu na vilevile kutumia huduma zetu mbalimbali nzuri na za haraka kama, kuweka amana zao, huduma za mikopo, kusafirisha pesa nje ya nchi, kutumia huduma za western union, kulipia kodi kwenye matawi yetu na huduma mbalimbali,” alisema Moshingi.

Aliongeza kuwa benki hiyo inaendelea kuboresha huduma zake, kupitia mpango mkakati wa 2012-2015, ambapo uboreshaji wa matawi anuai, kama matawi ya Kariakoo, Sumbawanga, na Ilala tayari umekamilika na uboreshaji zaidi wa
huduma za kibenki kupitia simu za mkononi yaani TPB Popote umeimarishwa na hivi sasa wateja wa benki hiyo wanaweza kuweka na kutoa fedha kwenye mawakala wa M-Pesa, Airtel Money na Tigo Pesa.

“Benki kwa mwaka huu 2013 imejipanga zaidi katika kukamilisha mikakati yake iliyoanza mwaka jana, ya kufanya mageuzi makubwa yakiwemo kukarabati baadhi ya matawi yake, kuongeza ufanisi, kupanua na kuboresha zaidi huduma za wateja, na kutumia Technologia ya TPB Popote na POS (Point of sales) kuwafikia wateja wetu popote pale walipo nchini Tanzania,” aliongeza.

Akizungumzia usalama wa fedha za wateja kufuatia tishio la wizi wa fedha kimitandao, Mkurugenzi wa Teknolojia na Uendeshaji wa benki hiyo, Jema Msuya alisema kwa benki ya Posta imejiimarisha zaidi hivyo hakuna tishio la wizi kupitia mitandao.

“Sisi tunamfumo mzuri wa kutoa taarifa kupitia teknolijia ya simu ya mkononi, tukio lolote linapotokea kwenye ankaunti ya mteja muda huo huo unapewa taarifa kupitia simu yako…sasa hakuna mwizi anayependa kufanya uhalifu na taarifa zitolewe muda huo huo…hii inatusaidia fedha za mteja kuwa salama muda wote,” alisema Msuya.

*Imeandaliwa na www.thehabari.com

Popular Posts