Pages

Friday, November 23, 2012

Sakata la Ununuzi wa Mitambo ya Dowans: Barua ya Zitto kwa Watanzania


Zitto Kabwe 
NDUGU Watanzania, 
r Ninawaandikia barua hii ya wazi kujieleza kwenu kuhusu mjadala mkali
uliolitikisa taifa siku chache zilizopita, kuhusiana na suala la maombi ya
Shirika la Umeme (TANESCO) kununua mitambo ya kuzalisha umeme ya Dowans. 
Mjadala ambao ulileta maneno na hisia nyingi sana katika jamii na miongoni
mwa wanajamii. Hisia nyingine ziligusa uadilifu wangu binafsi na hivyo
kutia mashaka imani kubwa ambayo Watanzania wamekuwa nayo kwangu na hata
kwa chama changu. 
Haya ni maelezo yangu mwenyewe, nimeandika mwenyewe ili kuwasiliana nanyi.
Kwa maelezo haya wananchi wafanye uamuzi na kunihukumu. Baada ya maelezo
haya sitasema tena kuhusiana na suala hili. 
Kwa muda sasa kumekuwa na mjadala mkali sana nchini kuhusu suala la uamuzi
wa TANESCO kununua mitambo iliyotumika ya kuzalishia umeme inayomilikiwa na
Dowans. 
Mjadala huu umehusisha TANESCO, Bunge (kamati mbili za Bunge, ile ya
Nishati na Madini na ile ya Hesabu za Mashirika ya Umma - (PAC), serikali
na watoa maoni - umma (public opinion makers). 
Itakumbukwa kuwa Desemba 14, 2008, serikali iliwasiliana na Kamati ya
Nishati na Madini ili kuijulisha nia yake ya kununua mitambo ya Dowans. 
Kamati ya Nishati na Madini ilitoa ushauri wa kukataa ombi hilo la
serikali. Uamuzi huo ulitangazwa na kamati kupitia vyombo vya habari
mbalimbali. 
Wakati huo, mimi na wenzangu wa CHADEMA tulikuwa jijini Mbeya kwenye kazi
ya Operesheni Sangara na niliposikia uamuzi huo, nafsi yangu ilijiuliza kwa
nini wameamua hivi? 
Nchi inahitaji umeme sana na hata nilipoulizwa na waandishi nini maoni
yangu, jibu langu lilikuwa ni la jumla sana, kwani niliamini kwa dhati
kabisa, mwisho wa siku nishati ya umeme ni muhimu sana kwa taifa na hivyo
kuna haja ya kupima mambo kwa undani zaidi. 
Mjadala huu haukuendelea sana. Serikali ilitangaza baadaye kuachana na
uamuzi huu wa kuingia zabuni ya kununua mitambo ya Dowams. 
Mnamo Januari 21 mwaka 2009; Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya
Umma, ambayo mimi ni Mwenyekiti wake iliwaita TANESCO ili kushughulikia
hesabu zao kwa mujibu wa kanuni za Bunge toleo la 2007. 
Hesabu zilizoshughulikiwa na kamati yangu ni hesabu za TANESCO zinazoishia
Desemba 2007. Kulikuwa na mambo kadhaa ambayo yalijitokeza katika hesabu
hizo. 
Mosi, TANESCO walikuwa wamepata hati safi ya ukaguzi. Kamati iliwapongeza
TANESCO kwa kuboresha kwa kiasi kikubwa vitabu vyao vya hesabu. 
Ikumbukwe kuwa TANESCO ilikuwa chini ya menejimenti ya Wazungu wa Net Group
Solution toka mwaka 2002. Katika hesabu za TANESCO zinazoishia Desemba
mwaka 2006, Mkaguzi wa Hesabu alishindwa kutoa maoni, kwani TANESCO
walikuwa na hesabu mbovu sana na hivyo kupata “disclaimer audit opinion.” 
Kitendo cha menejimenti ya Watanzania kusafisha uozo na kupata hati safi
ndani ya mwaka mmoja kilistahili pongezi. 
Bado ninatoa pongezi hizo kwa menejimenti ya TANESCO na wafanyakazi wote wa
TANESCO kwa kufanya kazi kwa bidii. 
Mimi huwa ninafurahia sana (excited) matokeo mazuri ambayo Watanzania
hufanya. Licha ya matatizo mbalimbali ambayo mashirika ya umma wanayo,
ninapoona kuna juhudi zimefanyika kufanya jambo jema, huwa ninaona raha
sana. 
Kwa kweli, juhudi hizi za kusafisha vitabu vya TANESCO, zilinijengea imani
kubwa sana na menejimenti ya TANESCO na kuona hawa watu wanaweza kutusaidia
kama nchi kutatua tatizo la nishati ya umeme. 
Pili, kamati ilipatwa na mshituko mkubwa sana kuhusiana na gharama za
uzalishaji wa umeme. Hili nimelizungumza pia katika mahojiano yangu na
baadhi ya waandishi wa habari kabla sijasafiri kwenda nje ya nchi. 
Asilimia 42 ya umeme wa TANESCO unanunuliwa kutoka kwa wazalishaji wa umeme
(Independent Power Producers – IPP). Hesabu ambazo kamati ilizipitia ni za
Desemba 2007 na hivyo kulikuwa na makampuni mengi sana ambayo yalikuwa
yanauza umeme kwa shirika letu. 
TANESCO walikuwa wananunua umeme kutoka Dowans na makampuni mengine ya
uzalishaji umeme kama Songas, Aggreko na IPTL. Mkataba wa Dowans na TANESCO
ulivunjika Agosti mwaka 2008; na ule wa Aggreko ulikwisha Oktoba mwaka huo
huo, yaani 2008. 
Makampuni haya mawili yalikuwa yanazalisha jumla ya 140MW za umeme na
kuingiza katika Gridi ya Taifa. Hivyo kuondoka kwake kuliondoa umeme mwingi
sana kutoka kwenye gridi. 
Pamoja na kwamba TANESCO wanazalisha asilimia 58 ya umeme wote unaozalishwa
nchini, lakini wanatumia asilimia 84 ya mapato yao kununua umeme. 
Yaani katika kila shilingi 100 ambazo wanapata, shilingi 84 wananunua umeme
na shilingi 16 tu ndio zinatumika kwa kazi nyingine kama kulipa mishahara
ya wafanyakazi, kukarabati njia za umeme na kuzalisha na kusambaza umeme
zaidi kwa watu wengine. 
Hili mimi binafsi niliona ni tatizo kubwa sana. Niliona ni tatizo ambalo
suluhisho lake ni kuongeza uwezo wa TANESCO kuzalisha umeme zaidi.
Vinginevyo itachukua karne Watanzania wengi kupata nishati hii muhimu sana
katika juhudi za kuleta maendeleo. 
Nchi yetu ni moja ya nchi ambazo usambazaji wa umeme upo chini sana.
Taarifa za kitafiti (Household Budget Survey 2007) zinaonyesha kuwa katika
kila nyumba 100 nchini, ni nyumba 12 tu zina umeme. Tena si umeme wa
uhakika. 
Hivyo, shirika la umma lenye jukumu la kuhakikisha kuwa Watanzania wanapata
huduma hii muhimu linapotumia zaidi ya theluthi tatu ya mapato yake kununua
chini ya nusu ya umeme unaosambazwa, linakuwa hatarini. 
Hali hii Watanzania wengi hawaijui kwa sababu viongozi wetu hawatwambii,
maana moja ya sababu iliyotufikisha hapo ni maamuzi yetu sisi wenyewe. 
Kamati yangu iliona kuna haja kubwa sana kupata majibu ya menejimenti ya
TANESCO kuhusu hali hii. Baada ya kupata majibu ya TANESCO ambayo yote yapo
kwenye kumbukumbu za Bunge (Hansard), kamati iliwaagiza walete taarifa ya
hatua wanazochukua kupunguza gharama na kuongeza mapato ili shirika liweze
kupata faida na kuondokana na hasara. 
Februari 21 mwaka 2009 TANESCO walikuja mbele ya kamati ili kutoa maelezo
yaliyohitajiwa na Kamati ya POAC. Walieleza masuala mbalimbali juu ya hali
ya nishati ya umeme nchini na hatua mbalimbali ambazo wanachukua ili
kukabili hali hiyo. 
Walieleza mikakati ya muda mrefu, muda wa kati na ya muda mfupi. Walieleza
pia mikakati ya dharura ili kupunguza nakisi ya umeme iliyopo hivi sasa
hapa nchini. 
Hivyo walielezea nia yao ya kununua mitambo ya Dowans ili kuongeza umeme
wanaozalisha wenyewe na pia kupunguza nakisi ya umeme iliyopo nchini. 
Walieleza nia yao ya kupeleka mtambo wa 60MW mkoani Mwanza ili kuweza
kukidhi hali ya uzalishaji wa umeme Kanda ya Ziwa, ambapo kuna ongezeko
kubwa la umeme kufuatia kuanza kazi kwa mgodi wa Buzwagi na kuunganishwa
mgodi wa North Mara kwenye gridi ya taifa. 
Mtu akipata fursa ya kusoma taarifa za Bunge, ataona maswali ambayo kamati
iliwauliza TANESCO. Maswali magumu sana. Haikuwa tu walikuja na kupewa
watakacho. Hapana. 
Kamati ikawauliza kwa nini kamati nyingine ya Bunge ya Nishati na Madini
iliwakataza kununua mitambo hii, wakajibu kuwa kamati hiyo haikuwapa nafasi
ya kujieleza. 
Nimesikia Mwalimu wangu, Dk. Harrison Mwakyembe, akisema kamati
iliwasikiliza. Napenda Watanzania wajue kuwa kuna taratibu za watu kuongea
na wabunge. 
Kulikuwa na mwakilishi wa TANESCO wakati Waziri wa Nishati na Madini
alipokutana na Kamati ya Nishati na Madini. Mwakilishi huyu hakuzungumza
kwani kamati ilipomaliza kumsikiliza waziri ikawatoa nje na ilipowarudisha
ikatoa msimamo wake. TANESCO hawakusikilizwa na kamati ya kisekta. 
Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma ikaazimia kuwa suala hili lina utata
ni vema kamati mbili za Bunge zikutane na kujadili na kufikia muafaka wa
pamoja. 
Tulitumia busara hii kama viongozi ili kuepuka kuchukua uamuzi unaopingana
na kamati nyingine ya Bunge. 
Sisi kama kamati yenye mamlaka ya kikanuni kuangalia ufanisi wa mashirika
ya umma, tungeweza kutoa maoni yetu tofauti na kamati nyingine. 
Wala hili si suala geni bungeni, kwani hata ndani ya kamati moja, wajumbe
hutofautiana na wengine kutoa maoni tofauti (kumbuka kesi ya Mengi na
Malima na uamuzi wa Anne Kilango Malecela na Christopher ole Sendeka). 
Mimi binafsi nilikataa kulifikisha Bunge katika hali ya kuonekana
kugawanyika kama ilivyo sasa. Ni wazi kuwa Kamati ya POAC ilikubaliana na
hoja za TANESCO juu ya umuhimu wa kununua mitambo ya Dowans lakini ikataka
kupata maoni ya kamati ya kisekta. 
Hili ni suala la kawaida sana kwa mabunge ya Jumuiya ya Madola kwa kamati
moja kukutana na kamati nyingine. 
Hata hapa nchini mara nyingi sana Spika wa Bunge amekuwa akitoa fursa kwa
kamati za Bunge kujadili mambo ambayo kimsingi ni ya Bunge zima ili
kuboresha shughuli za Bunge. 
Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma imekuwa na kawaida ya
kushirikisha wabunge wengine kutoka kamati nyingine katika kazi zake
mbalimbali ili kuboresha mawasiliano ndani ya Bunge na kuhakikisha kuwa
wabunge tunakuwa na habari zinazofanana. 
Kuna mifano miwili napenda kuiweka wazi hapa ili Watanzania wajionee
wenyewe mtindo wangu huu wa kushirikisha kamati nyingine kwenye kazi za
Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma. 
1. Kamati ilifanya ziara kutembelea kiwanda cha Sukari cha Kagera na
kuongozana na wajumbe wa Kamati ya Fedha na Uchumi na Kamati ya Maendeleo
ya Jamii (kwani mifuko ya hifadhi ya jamii ipo katika kamati hizi mbili). 
Madhumuni ya ziara hii yalikuwa ni kujiridhisha na uamuzi wa mifuko ya
hifadhi ya jamii kukopesha Kampuni ya Sukari ya Kagera mabilioni ya fedha. 
Kazi hii ni kazi ya kimahesabu kwa kamati yangu, lakini kwa busara za
kiuongozi niliwasiliana na Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Uchumi,
Abdallah Kigoda na wa Kamati ya Maendeleo ya Jamii, Jenista Mhagama, ili
kupata ushiriki wa kamati zao. 
Mifuko hii pia kwa masuala ya kisera hukutana na kamati hizi na hivyo
ushiriki wao ulikuwa unapanua mawasiliano ya kikamati. 
2. Kamati ilifanya ziara nchini Kenya na Afrika Kusini na kuongozana na
wajumbe wa Kamati ya Maliasili (kwani TANAPA ipo kwenye kamati hii). 
Lengo la safari ilikuwa kuona jinsi wenzetu wanavyoshughulikia hesabu za
taasisi za uhifadhi ili kuhakikisha kuwa uhifadhi wa wanyamapori unafanyika
kwa tija bila bugudha ya serikali kuu kuchota fedha kutoka kwenye taasisi
za hifadhi. 
Kamati yangu iliwasiliana na Mwenyekiti wa Kamati ya Maliasili na kupata
uwakilishi wa kamati hii katika kazi za Kamati ya Hesabu. 
Hii yote ni kuonyesha umuhimu wa kamati za Bunge kufanya kazi pamoja. Kwa
‘spirit’ hii hii kamati ilitaka kamati mbili zikutane kuhusu hoja za
TANESCO kabla ya kushauriwa vinginevyo na Katibu wa Bunge. Katibu wa Bunge
aliniambia kuwa kamati mbili zisikutane. 
Nilishtushwa kusoma katika vyombo vya habari (nikiwa ughaibuni nchini
Suriname) kuwa Spika amekataa kamati kukutana, akijua kabisa kuwa hapakuwa
na ombi hilo mezani kwake la kamati mbili kukutana, kwani tayari nilikuwa
nimefuata ushauri wa Katibu wa Bunge na kuandika maoni ya kamati kwa Waziri
wa Nishati na Madini. 
Nakala ya barua yangu ipo Ofisi ya Bunge na kama Spika angepata japo nafasi
ya kusoma barua ya Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma kwa
Waziri wa Nishati na Madini (ambayo imeandikwa kwa mujibu wa kanuni za
Bunge na kwa ushauri wa Katibu wa Bunge) ninaamini asingeyasema aliyoyasema
kwenye mkutano wake na vyombo vya habari. 
Binafsi ninashindwa kuelewa Kamati ya Nishati ya Madini ina nini kwani
wametaharuki sana na suala hili. 
Hii inadhihirishwa na kitendo cha wao kumpigia spika simu na kumueleza kuwa
kamati yetu imeamua mitambo ya Dowans inunuliwe ilhali kikao kilikuwa bado
kinaendelea na hata ajenda ya Dowans haikuwa imefikiwa. 
Spika naye alimtuma Katibu wa Bunge kuja kwangu kuulizia. 
Nilichofanya ni kumfungulia mlango katibu na kumuonyesha kuwa hata kikao
hakijaisha, tutakuwaje tumeamua? 
Nataka nieleze waziwazi mbele ya umma na nihukumiwe kwa maamuzi (judgement)
yangu kwamba nilikubaliana na hoja za TANESCO za kutaka kununua mitambo ya
Dowans. 
Ninaamini kuwa hoja zao ni za kitaalamu na ni sahihi. Ni hoja ambazo
hazijibiwi kwa maelezo ya kisiasa tu na vita takatifu dhidi ya ufisadi
iliyoanzishwa na chama changu cha CHADEMA. 
Kuna hoja mbalimbali ambazo zinatolewa kupinga ununuzi huu, ikiwamo hoja ya
kwamba sheria ya manunuzi ya umma ya mwaka 2004 inakataza. 
Hakuna hata kipengele kimoja cha sheria ya manunuzi kinachokataza ununuzi
wa mitambo iliyotumika. 
Bahati mbaya sana wananchi wamelishwa sumu kali sana kuhusu suala hili na
waandishi na wataalamu wa kutoa maoni bila hata kuuliza sheria gani ya
manunuzi? 
Hakuna hata mtu mmoja aliyediriki kutaja kipengele cha sheria ya manunuzi
ya 2004 iliyotungwa na Bunge inayokataza kununua vifaa vilivyotumika. 
Hata hivyo, kanuni za manunuzi, kanuni 58 (3) ndiyo inakataza na kanuni
hutungwa na waziri mwenye mamlaka na kuchapishwa katika gazeti la serikali
(GN). 
Hivyo kama serikali inaona kuna suala la msingi kwa taifa inatoa ‘waiver’
kwa kanuni hii na suala hilo kutekelezwa. Sheria ya manunuzi imetumika tu
kama kigezo cha wanaopinga mitambo hii kununuliwa bila kujali kuwa huko
tunakokwenda kama taifa twaweza kukutwa na mazingira ambayo itatupasa
kununua vifaa ambavyo si vipya. 
Mzee Thabiti Kombo, alikuwa akisema, tuweke akiba! Si akiba ya fedha, akiba
ya maneno. Viongozi ni lazima kuzingatia sana hili tunapokuwa tunajenga
hoja zetu kusapoti misimamo yetu, kwani hoja hiyo hiyo yaweza kukuzuia
kufanya maamuzi mengine muhimu kabisa kwa taifa. Tuweke akiba, viongozi! 
Kuna wanaotoa maoni kuwa hii ni mitumba tu, isinunuliwe, Prof. Ibrahim
Lipumba, mchumi mwenzangu amezungumza juu ya suala hili vizuri. 
Hii nchi inayoendelea mitambo mikubwa kama ya madini, umeme na mingineyo
yaweza isiwe mipya. 
Sekta binafsi na hasa kwenye maeneo ya miundombinu hutumia sana vifaa
vilivyokwisha kutumika. 
TANESCO lazima liwe shirika ambalo linajiendesha kibiashara, huwezi kulipa
masharti ya kimanunuzi sawa na wizara ambayo yenyewe kila mwaka unaipa
bajeti. Shirika linapaswa kufanya maamuzi kibiashara. 
Leo, tumeiondoa Stamico katika orodha ya mashirika yanayotakiwa
kubinafsishwa ili washiriki kikamilifu katika sekta ya madini. Shirika la
NDC tumelipa jukumu kubwa la kuendeleza Mchuchuma na Liganga. 
Hawa hawatatumia mitambo mipya tu. Kuna migodi inafungwa sehemu mbalimbali
za dunia na vifaa vyake vinahamishwa kupelekwa sehemu nyingine. 
Hali ni hiyo hiyo kwenye sekta ya nishati. Haya maneno ya kisiasa
yanayodakwa kwa kiasi kikubwa na hata baadhi ya wasomi, yatakuja
kuligharimu taifa. 
TANESCO wamefanya utafiti wa kitaalamu, ingepaswa Bunge kama lina mashaka
lingetoa zabuni ya mtaalamu kufanya ukaguzi huru na kutoa ripoti yake.
Unapinga maelezo ya kitaalamu kwa taarifa za kitaalamu. 
Si taarifa za kina Selelii, eti tu kwa sababu walikuwa wajumbe wa Kamati ya
Richmond. Hapana. Mataifa hayaongozwi namna hii. 
Watanzania, Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO amesema inachukua muda kununua
mtambo mpya, kwani huchukua muda wa kutoa order, kuunda, kusafirisha,
kufanya majaribio, kukamisheni na baadaye kuanza kuzalisha. Wanasiasa aah,
mbona Dowans walichukua muda mfupi? 
Sote tumeshasahau kuwa mitambo waliyoleta Richmond ilikuwa inatumika kwenye
michezo ya Olimpiki kule Athens, Ugiriki na hivyo walinunua mitambo ambayo
ilikuwa imeshatumika, ndiyo maana muda ulitumika mfupi. 
Kama TANESCO watanunua mitambo iliyotumika tofauti na ile ya Dowans, hili
la haraka litawezekana. Isipokuwa itakuwa ni mitambo iliyotumika. 
Ni vema tutambue kuwa TANESCO, wamepanga kununua mitambo hii kwa kuwa ni
suala la dharura. 
Suluhisho la kudumu la uzalishaji wa umeme ni kumaliza miradi ya Mtwara
300MW, Kinyerezi 240MW na Ruhudji 350MW. 
Vilevile ni kununua IPTL na kuigeuza kuwa gesi ili kupunguza gharama za
kununua umeme. Miradi kama Stigler’s gorge nayo imo kwenye mipango ya nchi.
Lakini kupanga ni kupanga, utekelezaji ni suala jingine. 
Miradi yote hii ukiwamo ule wa Kiwira 200MW imekwama kwa sababu mbalimbali,
ikiwemo vita dhidi ya ufisadi ambayo tunaendelea nayo. Ni ukweli
usiopingika kuwa tupo kwenye tatizo kubwa la nishati ya umeme na ni lazima
tupate ufumbuzi wa muda mrefu, wa kati na mfupi. 
Mimi naanza kupata wasiwasi kuwa hii vita dhidi ya ufisadi ambayo
ilianzishwa na CHADEMA na wabunge wa CCM aina ya Mwakyembe kuidaka inaanza
kupoteza mwelekeo. 
Vita dhidi ya ufisadi si “witch hunting”. 
Vita dhidi ya ufisadi ni vita takatifu ambayo lazima itende haki.
Hatuendeshi vita dhidi ya ufisadi ili kuridhisha makundi fulani na kukomoa
kundi fulani la kisiasa. Hii si vita ya visasi hata kidogo. 
Nchi ni zaidi ya vita dhidi ya ufisadi. A country must move forward.
Hatuwezi kurundika sababu zote za umaskini wetu kwenye ufisadi, lazima
tutambue kuwa matatizo tuliyonayo sasa ya nishati ya umeme ni matokeo ya
makosa ya kisera tuliyoyafanya huko nyuma. Ninatumia neno tuliyoyafanya,
maana hapa sasa ni letu wote. Tulifanya makosa ya kisera. 
Sera ya ubinafsishaji iliyoliweka Shirika la TANESCO kwenye orodha ya
kubinafsishwa (specification) ndiyo imesababisha TANESCO kuwa katika hali
hii tuliyonayo. 
Wakati tunachukua maamuzi haya ya kishenzi wanaopiga kelele kuhusu ufisadi
hivi sasa (walokole wa vita ya ufisadi) ndio walikuwa watendaji serikalini. 
William shellukindo, mzee ninayemheshimu sana sana katika duru za kibunge,
alikuwa Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, mratibu mkuu wa sera za serikali. 
Baadaye mzee Shellukindo akawa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Mashirika
ya Umma. Mimi nilikuwa shuleni wakati huo. Sikumsikia anapinga na hivyo
kuliokoa taifa na hata kufikia hapa tulipofikia. 
Wakati tunafanya maamuzi haya ya kishenzi ya mashirikiano yetu, kina Dk.
Mwakyembe ndio walikuwa marafiki vipenzi wa Rais Mkapa (blue eyed boys) na
hawakumkatalia alipoleta Netgroup Solution baada ya miaka mitano ya
kuhujumu TANESCO kama ‘A specified company.’ 
Hawa leo ndio wanamuuliza Dk. Rashidi alikuwa wapi mpaka kufikia kusiwe na
umeme wa kutosha. Mimi nawauliza wao walikuwa wapi mpaka nchi kufikia hali
hii? 
Walikuwa wapi walipoamua kuwa serikali haiajiri na hivyo tuna crisis kubwa
katika utumishi wa umma, kwa sababu ya ombwe la miaka 10 ya kutoajiri na
hivyo makatibu wakuu na wakurugenzi wana hofu sasa wakiondoka nchi itakuwa
kwenye tatizo. 
Mwakyembe alisema Watanzania si mabwege. Ni kweli sisi si mabwege.
Watanzania pia si mandondocha ambao hawajui walikotoka na wanakokwenda! 
Viongozi wa Kamati ya Nishati na Madini wanataka Watanzania waamini kuwa
matatizo tuliyonayo ya umeme yamesababishwa na Richmond na Dowans. Mimi
ninakataa. 
Kamati ya Nishati na Madini ya Bunge imefanya nini kuhusu Kampuni ya ALSTOM
POWER RENTALL, ambayo imelipwa sh bilioni 30 bila kuzalisha umeme hata unit
moja mpaka inamaliza mkataba wake? Kamati hii ni ya Richmond au Dowans tu?
Mimi si ndondocha. Nipo tayari kuwa peke yangu. 
Viongozi wanaowaambia wananchi wanayotaka kusikia na kuogopa kufanya
maamuzi. Viongozi wanaotoa majibu mepesi kwenye matatizo ya msingi ya nchi
hawana tofauti sana na Adolf Hitler. 
Leo tukiwa na tatizo la msingi kabisa kuna watu watasema, mafisadi hao,
ilimradi kupata wa kumlaumu. 
Matokeo yake tunashindwa kutatua matatizo yetu ya msingi. Sababu kubwa ya
Hitler kupata madaraka Ujerumani ilikuwa uwezo wake wa kutoa majibu matamu
kwa maswali magumu. 
Ni rahisi sana kusema tatizo la umeme chanzo ni mafisadi. Baadaye watasema
tukipata madaraka tutakata vichwa mafisadi wote na nchi itakuwa sawa. Mungu
apishe mbali. 
Kuna ‘fundamentals’ za nchi haziko sawa ndiyo maana nimekuwa nikiomba
tujenge national consesus (mwafaka wa kitaifa). Huwezi kumaliza tatizo la
nishati ya umeme nchini kwa kusema, ‘ufisadi huu jamani.’ 
Ni lazima viongozi tukae chini na kufanya maamuzi magumu. Huwezi kuwa
kiongozi ambaye siku zote unafanya maamuzi ‘popular’ ili ushangiliwe.
Lazima uwe tayari kuzomewa, kutukanwa na kukashifiwa ili mradi uamue jambo
unaloamini ni jema. 
Hili la TANESCO kununua mitambo ni jambo jema ili tuongeze uwezo wa nchi
kuzakisha nishati ya umeme. Kama kungekuwa na ufisadi, Dowans/TANESCO
wangehonga kamati yangu au mimi binafsi. Sijaona kiongozi wa TANESCO au
Dowans aliyenifuata ili kamati iamue kuwapendelea. Sijamwona. 
Ninajua imani ya wananchi kwa wanasiasa ni ndogo sana. Imani ya Watanzania
wenyewe kwa wenyewe ni ndogo sana. Utafiti wa serikali (PHDR 2007)
unaonyesha asilimia 78 ya Watanzania hawaaminiani. 
Hivyo ni sahihi kutoamini. Ni sahihi kuwa na mashaka. Hata hivyo mimi
naamini kuwa suala hili ni jema kwa nchi. 
Katika mahojiano ya Dk. Mwakyembe na ITV na baadaye kuandikwa na vyombo vya
habari, alisema kuwa kamati yangu ilipewa posho kubwa ili kupitisha suala
hili la Dowans. 
Nimeshtushwa sana na kauli hiyo na kwa kweli ni kauli ambayo lazima
ifanyiwe kazi na vyombo vya dola. 
Nimemwandikia barua, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU na kumuomba afanye
uchunguzi rasmi kwa wajumbe wote wa kamati yangu kama walipata posho yoyote
ambayo hawakustahili katika kikao hicho kilichojadili suala la Dowans. 
Tuhuma za kuhongwa si kitu cha mchezo na kuachwa tu. Ninachukia sana hongo.
Ni muhimu suala hili kuchunguzwa. 
Nimesikia Dk. Mwakyembe akisema yote niliyosema ni yangu binafsi na si ya
kamati. Nimeshtushwa, imekuwaje Dk. Mwakyembe amejua kuwa niliyosema si
maamuzi ya Kamati ya POAC ? 
Inawezekana kuna wajumbe wenzangu wamemwambia kuwa hayakuwa maamuzi ya
kamati. Hili nalo si jambo jema kwa mwenyekiti yeyote wa kamati ya Bunge. 
Nimeamua, mara kamati itakapokutana kwa ajili ya vikao vyake, nitawaomba
wajumbe wa kamati wapige kura ya kutokuwa na imani na mimi. Siwezi kuongoza
kamati ambayo sisimamii maamuzi yake au yenye mgawanyiko ndani yake. 
Iwapo nitashindwa kura hiyo ya kutokuwa na imani nami, nitajiuzulu
uenyekiti wa kamati mara moja. 
Iwapo nitashinda kura hii ya kutokuwa na imani nami, nitamtaka Dk.
Mwakyembe, aniombe radhi kwa mtindo ule ule aliotumia kusema kuwa maamuzi
niliyoyasema si ya kamati bali ni yangu binafsi. 
Hatuwezi kuwa na viongozi wanaoropoka kila linalowajia mdomoni ili kutimiza
matakwa yao ya kisiasa. 
Nimekulia kwenye harakati za kisiasa. Nimelelewa katika malezi ya kidini na
baadaye kijamii kupitia walimu wangu kama marehemu Profesa Chachage,
Profesa Issa Shivji, Profesa Haroub Othman na Dk. Azaveli Lwaitama. 
Walimu wangu hawa ambao huwachukulia kama wazee wangu, watakuwa ni moja ya
watu ambao mjadala huu umewaumiza sana. 
Hii ni pamoja na wanaharakati wengine wengi na hasa mama zangu wa Mtandao
wa Jinsia Tanzania (TGNP) ambao walinilea tangu nikiwa chuo kikuu. 
Viongozi wangu wa CHADEMA na hasa wazee wangu, Mzee Mtei, Makani, Masinde,
Prof. Baregu na wengineo, watakuwa kwenye simanzi kubwa na kujiuliza kijana
wetu huyu amepatwa na nini? 
Wanachama wa CHADEMA nchi nzima wana maswali mengi vichwani mwao juu ya
sakata hili. Vijana wa Tanzania ambao wamekuwa wakiniona kama ‘role model’
wao wametaharuki na sakata hili na hata wengine kuona wamenipoteza katika
harakati. 
Ninawaomba radhi kwa kuchukua uamuzi ambao wengi hamjaupenda. Uamuzi ambao
kwa habari nilizopewa ninauona ni sahihi. 
Ninaamini kuwa si mara zote mtu unayempenda huchukua uamuzi unaoupenda.
Mara hii nimechukua uamuzi ambao ninaona ni muhimu kwa taifa, lakini
haupendwi na wengi. 
Ninaomba mnielewe. Hili ni jaribio la kiuongozi. Hii ni gharama ya uongozi.
Gharama ambayo nipo tayari kuibeba. 

Popular Posts