Pages

Monday, August 13, 2012

MAONI YA KATIBA MPYA-MTAZAMO WA WAKRISTO

WALA MSIACHE KUTUMIA AKILI ZENU IPASAVYO!!

MFUMO WA KUITAWALA: Tuendelee na mfumo wa Kisekula na wa kijamhuri katika kuongoza, kutawala na kuendesha shughuli zote za nchi, kama ilivyo sasa, sawa na Ibara 3 (1) ya katiba iliyopo sasa.

1. MIFUMO YA KI-DINI, KI-KABILA NA YA UBAGUZI WA AINA YOYOTE ISIINGIZWE KATIKA KATIBA. Kulingana na hali iliyopo sasa, dalili za wazi zimeanza kujitokeza kwa baadhi ya Viongozi kuwa watiifu kwa Imani zao na wengine jinsia, ukabila na sehemu wanakotoka badala ya kuzingatia utaifa na Utanzania wao. Mifano ni pamoja na:-

a) Kurudishwa kwa Mahakama ya kadhi na serikali kuamua kugharimia masomo ya viongozi wake kinyume kabisa na Ibara ya 19(2), kama Waziri Mkuu alivyotamka hivi karibuni.

b) Matamshi ya Waziri wa Katiba, Zanzibar kutaka watu wote wageni na wenyeji kutii sheria za Kiislamu zinazohusiana na mfungo wa mwezi wa Ramadhani – akikiuka kifungu cha (1) cha Ibara hiyo ya 19 ya katiba iliyopo sasa.

Ibara ya 19 (1) inasema: Kila mtu anastahili kuwa na uhuru wa mawazo, Imani na Uchunguzi katika mambo ya dini, pamoja na uhuru wa mtu kubadilisha dini au Imani yake.

19(2) nayo inasema: Kazi ya kutangaza dini, kufanya ibada na kueneza dini itakuwa ni huru na jambo la hiari la mtu binafsi , na shughuli na uendeshaji wa jumuiya za dini kufanya zitakuwa nje ya shughuli za mamlaka ya nchi.

Kutoka na maamuzi ya Serikali yaliyotamkwa kupitia Waziri Mkuu, na matamshi ya Waziri wa katiba Zanzibar, tunaona kuwa hata yale mambo ya ki-ibada, mfano:

a) Kulazimisha uvaaji wa sare zinazoonyesha dini au imani au ubaguzi wa aina fulani katika mashule, vyuo na taasisi mbalimbali za Serikali na za umma.

b) Kulazimisha majengo ya ibada katika mashule, vyuo na taasisi mbalimbali za Serikali na za Umma.

c) Kulazimisha uchinjaji wa wanyama na ndege kufavywa na waislamu peke yao na wengine kuonekana haramu.

Haya yote ni uvunjifu wa katiba iliyopo, kukiuka haki za watu wengine katika uhuru wa kuabudu na pia yanaleta mgawanyiko katika Taifa.

Kama Serikali haikuangalia kwa makini jambo hili, punde si punde, machifu nao watataka kurudishiwa mamlaka zao za uchifu, mamlaka za kidini hasa sisi Wakristo tutataka kurudishiwa mali zetu zilizotaifishwa na kudai kuwa na Mahakama zetu chini ya Waamuzi kama Biblia inavyobainishwa – nazo zigharimiwe na Serikali.

3.UENDESHAJI WA TAASISI ZA SERIKALI NA SERIKALI ZENYEWE.

· Katiba ya nchi itamke na kuheshimiwa na wote tupewe dhamana kulinda na kuitetea.

· Mambo ya dini yoyote yasipenyezwe kwa siri au kwa wazi katika kuendesha vyombo vya Umma (Dola, Mbunge na Mahakama)

· Kiongozi yeyote akionekana kufanya upendeleo huo kinyume na Katiba ashitakiwe na kuondolewa katika utumishi huo.

· Kukatisha kazi za Serikali ili kutoa mwanya kwa mambo ya dini moja ni upendeleo na si haki jambo hilo lisifanywe kabisa.

· Serikali isiruhusu au kushabikia mvutano wa kidini ama ushindani ambao unaweza kuleta vurugu katika nchi.

4. MAMBO YA MUUNGANO.

· Kupokezana Urais kati ya Tanzania ya Zanzibar na Tanzania ya Bara, hili lisiingie katika katiba Mpya.

· Rais achaguliwa toka popote Tanzania kulingana na uzalendo wake kwa nchi, uwezo maadili (Sio kwa ubaguzi wowote wa rangi na dini.

· Tanzania Zanzibar kuna Wakristo lakini hatuwaoni kuwakilishwa katika simulizi kuwepo na usawa katika kuwapa nao fursa wasibaguliwe. Mfano Tume ya kukusanya maoni hakuna Mkristo yoyote kutoka Zanzibar

· Wakristo wa Zanzibar wasilazimishwe kutii sheria za kiislamu hasa mwezi wa Ramadhani maana wao kwao sio imani yao huo ni ubaguzi na Unyanyasaji.

5. SHERIA ZA DINI MBALIMBALI.

· Sheria za dini zenye mkazo wa imani ya dini fulani tu zisingizwe katika katiba mpya (zitaleta vurugu)

· Mfano: sheria za kiislam, kikristo (kikatoliki) kimila kitume ambazo hazilingani na mfano wa kisekula zisiingizwe katika katiba mpya

· Kuingizwa kwa sheria za dini moja au baadhi utaleta hisia za kidini na chuki cha kidini

· Waumini wa dini husika watii sheria zao kwa uhuru wao bila kulazimishwa au kulazimisha wengine wasio wa dini hiyo

· Mifumo ya kiuchumi yenye harufu ya kidini isiingizwe katika sera za uchumi wa taifa mfano mfumo wa benki za kiislamu zinawabagua wakristo

· Alama za kidini mfano mavazi yenye sura ya kiibada yasitumiwe ndani ya maeneo ya ibada wasiohusika wasilazimishwe kuzitumia kwa visingizio vyovyote vile (sare za hijabu mashuleni)

6. CHAGUZI MBALIMBALI

Kuwepo Tume huru yenye mamlaka kamili ya kusimamia uchaguzi

· Siku ya kupiga kura isiwe siku ya ibada kwa dini yoyote

· Mgombea binafsi aruhusiwe kwa ngazi zote hiyo ni haki ya msingi ya kila mtu

· Mgombea achaguliwe kwa kuzingatia sifa za uwezo, maadili na uzoefu

· Sifa za udini, ukabila,ukanda,rangi na nasaba zisihusike (katiba izikataze)

· Mgombea yeyote atakayetumia kampeni za udini au ushawishi wa kidini, ukanda,ukabila,ubaguzi wa rangi au nasaba afutwe kwenye ugombea.

7. MGAWANYO WA MADARAKA.

· Uzingatie uwezo wa mtanzania, maadili yake, uzoefu wake pekee.

· Usiwepo ubaguzi wa jinsi, rangi, hali, ukanda, kabila na udini.

· Uwiano wa kidini usiwepo kabisa kwa vile Serikali haina dini pia itaongeza chuki na migogoro isiyo na tija.

· Kupokezana madaraka kwa misingi ya udini usiwepo kwa vile dini nyingi na kila moja ina haki sawa hakuna dini iliyo juu ya nyingine katika mfumo wa kisekula.

8. UHURU WA KUABUDU.

· Uendelee kama ulivyo ainishwa katika katiba ya 1977 Ibara ya 19.

· Kila dini ijiendeshe yenyewe kwa gharama zake bila kuvunja sheria za nchi na kugandamiza makundi mengine.

· Kila dini iheshimu dini nyingine zilizosajiliwa kisheria

· Kila raia ana haki kuchagua dini anayotaka au kuhamia dini anayotaka asibughudhiwe (Hiyo ni haki ya kibinadamu)

· Serikali, Bunge na Mahakama ziheshimu na kulinda uhuru huo.

9. MAANGALIZO/HISIA ZETU KAMA VIONGOZI.

· Tumeona kidogo kidogo Serikali inaingiza mambo ya dini moja kwa kasi na kusahau kwamba kuna dini nyingi katika Tanzania zenye haki sawa, Je? Serikali itakuwa tayari kusikiliza na kuingiza madai ya kila dini katika katiba? Utekelezaji wake utakuwaje? Ikiwa haiwezi kupokea na kuyaingiza madai ya dini zote katika katiba tunashauri iache jambo hilo maana litaleta migogoro isiyoisha ndani ya nchi.

· Tunahisi Serikali inatumia ukimya wa wakristo kufikiri kwamba hawaoni, hawajui, hawajali na hawawezi kusema au wanaogopa? Ama hawana madai au sheria na kanuni za Kimahakama aidha tunahisi Serikali ina dini ingawa haijatamka rasmi maana kuna mambo yanayotokea sasa, yanayoashiria kuingiza mambo ya dini moja wanapolalamika bila kuzingatia athari katika dini zingine ( Kusitisha shughuli za Bunge kwa ajili masilahi ya wabunge wa dini moja).

· Tunahisi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni ya Kiislamu ndiyo maana nyumba za Ibada za wakristo zinachomwa moto kila mara na pia wakristo wa Zanzibar hawapati nafasi za uongozi, mfano wajumbe katika Tume ya kukusanya maoni ya marekebisho ya Katiba wajumbe wote 15 ni Waislamu kama kuna madai ya uwiano wa uongozi kwa misingi ya udini mbona huko hauzungumzwi?

HITIMISHO.

Tunatoa wito kwa wananchi wote:-

i. Tunaomba wananchi wote washiriki kutoa maoni bila woga mbele ya Tume ya kukusanya maoni yao, ni haki yao ya msingi

ii. Viongozi wa dini zote waaelimishe na kuwazuia waumini wao kupigania udini na itikadi za dini zao kuingia kwenye katiba inayoongoza watu wote wenye dini na wasio na dini, pia ni vizuri viongozi hao watamke hadharani kulinda na kutetea katiba ya nchi.

iii. Tunawaunga mkono Wabunge wanaopigania utaifa na maslahi ya watu wote tunawatia moyo waendelee kutetea mambo ya Kitaifa na hasa maslahi ya Watanzania wote tuko nyuma yao hata kama watazomewa Bungeni tunaomba wananchi wawaunge mkono na ikibidi kuwachagua uchaguzi ukifika endapo watagombea.

iv. Jambo lolote lenye itikadi za kidini au Kisiasa (Chama) lisiingizwe kwenye katiba kwa tafsiri inayoeleweka na upande mmoja hadi hapo tafsiri hiyo itakapo jadiliwa na pande zote husika na kujiridhisha kuwa halina madhara kwa maslahi ya Taifa.

v. Viongozi waliopo madarakani hivi sasa watamke hadharani ili Watanzania wajue misimamo yao katika kulinda na kutetea katiba, ikiwa ni pamoja na kutounga mkono mambo ya udini, ukabila, ubaguzi wa rangi, jinsia ili kuondoa hisia za watanzania kwamba wanatetea dini zao (Kinyume na walivyo apa) Ni wajibu wa wananchi kuwapima viongozi wote katika misingi hiyo ili kujua kwamba wanatenda haki au la.

vi. Pia tunatoa wito kwa watanzania wote bila kujali itikadi zao wajitokeze kuhesabiwa siku ya Sensa.


Chanzo : MAMBO YA MSINGI YA KUCHANGIA KATIKA KATIBA

Popular Posts