Pages

Thursday, September 6, 2012

Kilimanjaro Premium Lager yazipatia timu za Yanga na Simba vifaa vya Michezo kwa ajili ya Ligi Kuu

Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, George Kavishe akikabidhi sehemu ya vifaa hivyo vya michezo kwa Makamu Mwenyekiti wa timu ya Simba,Geofrey Nyange Kaburu.Katikati ni Mkurugenzi wa Mashindano wa TFF, Saad Kawemba
Picha ya Pamoja:Toka kulia ni Makamu Mwenyekiti wa timu ya Simba,Geofrey Nyange Kaburu,Mkurugenzi wa Mashindano wa TFF, Saad Kawemba,Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, George Kavishe na Afisa habari wa Timu ya Yanga,Luis Sendeu.
Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, George Kavishe akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa hafla fupi ya kukabidhi vifaa vya micheko kwa timu za Yanga na Simba za jijini Dar es Salaam iliyofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa Shirikisho la Soka nchini (TFF) Ilala.Kushoto ni Afisa habari wa timu ya Yanga,Luis Sendeu na kulia ni Mkurugenzi wa Mashindano wa TFF, Saad Kawemba.
Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, George Kavishe akikabidhi sehemu ya vifaa hivyo vya michezo kwa Afisa habari wa Timu ya Yanga,Luis Sendeu.

Zikiwa zimebaki siku tisa kabla ya kuanza kwa msimu wa ligi kuu Tanzania Bara 2012/2013, Kilimanjaro Premium Lager imezikabidhi timu za Yanga na Simba vifaa kwa ajili ya michuano hiyo.

Vifaa hivyo vimetolewa ikiwa ni sehemu ya udhamini wa jumla wa dola za Kimarekani milioni 3 (takribani TSh4bilioni) za kinywaji cha Kilimanjaro Premium Lager kwa timu hizo kongwe na zenye ushindani mkubwa na historia yakipee hapa nchini.Vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na jezi, kaptula, soksi, vyatu vya mpira, bibs, mipira na mifuko.

Akizungumza katika makabidhiano hayo, yaliyofanyika katika ofisi za Shirikisho la Mpira wa miguu Tanzania (TFF), Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, George Kavishe alisema:

“Ni dhahiri kuwa Simba na Yanga ni klabu kubwa zaidi nchini Tanzania na zote kwa pamoja zimetwaa ubingwa wa soka Tanzania Bara mara 40 (Yanga mara 22 na Simba mara 18), jambo ambalo ni mafanikio makubwa sana kwa timu hizi. Ni wazi kuwa hakuna timu nyingine iliyoweza kufikia historia hii ya pekee hapa nchini na kama mdhamini mkuu wa timu hizi, Kilimanjaro Premium Lager imeona umuhimu wa kuziunga mkono klabu hizi katika jitihada zake za kutuletea tena ushindani wenye burudani.” Alisema.

Pazia la michuano ya kuwania ubingwa wa mpira wa miguu Tanzania bara kwa msimu wa 2012/2013 litafunguliwa rasmi Septemba 15 mwaka huu kwa jumla ya timu 14 kujitupa kwenye viwanja tofauti.

Kavishe aliahidi kuwa kinywaji cha Kilimanjaro Premium Lager kitaendelea kudhamini timu za Yanga na Simba kutokana na ukweli kwamba timu hizo ndio zenye wapenzi wengi zaidi hapa nchini na zinazotoa wachezaji wengi zaidi katika kikosi cha timu ya taifa (Taifa Stars).

“Ushirikiano kati ya Kilimanjaro Premium Lager na klabu hizi umejikita katika mambo yanayotuunganisha kama vile ushirikiano, umoja na kujituma kufanya kilicho bora. Tunaendelea kutimiza wajibu wetu kwa klabu hizi na tuko tayari kupeleka mpira wa Tanzania kwenye kilele cha mafanikio,” alisema.

Popular Posts