
   Mwakilishi wa Timu ya Soka ya Kitope United akipokea msaada wa Seti ya  Jezi pamoja na Fedha Taslimu kwa ajili ya usajili na kujiandaa kwenye  mashindano yanayowakabili. 
 
   Makamu wa pili wa Rais Zanzibar na Mbunge wa Jimbo la Kitope Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na  wanamichezo wa Timu nne za soka za Jimbo la Kitope hapo ukumbi wa Tawi  la CCM la Kitope A. 
 
 Khamis Mswahili Mwinyi Mwakilishi wa wanamichezo wa timu nne za soka za  Jimbo la Kitope akiwasilisha changamoto wanazokabiliana nazo katika  michezo kwa Mbunge wa Jimbo hilo Balozi Seif Ali Iddi. 
  --
   Uongozi wa Jimbo la Kitope umekusudia kuimarisha sekta ya michezo kwa  lengo la kuwawezesha Vijana wa Jimbo hilo kuwa pamoja katika harakati  zao za Michezo na zile za kijamii. 
  Makamu wa pili wa Rais Zanzibar na  Mbunge wa Jimbo hilo Balozi Seif Ali Iddi alisema hayo mara baada ya  kupokea matatizo na ushauri wa wanamichezo wa Timu Nne zilizomo ndani ya  Jimbo hilo walioutoa katika Kikao chao kilichofanyika katika Ukumbi wa  Mikutano wa Ofisi ya Tawi la CCM Kitope A. 
   Balozi Seif aliwaeleza wawakilishi wa Timu hizo ambazo ni Kitope United,  African Boys, Home Boys na Kombora kwamba  uamuzi wao wa kufikiria  kuanzisha Timu moja imara ndani ya jimbo hilo umetoa faraja  kwa  viongozi jambo ambalo litarahisisha hata upatikanaji wa vifaa na misaada  kwa wepesi zaidi.
    Aliahidi kwa kuwa yeye ni Kiongozi wao wa Jimbo atahakikisha kwamba   Sekta ya Michezo inapata nguvu zaidi kutokana na umuhimu wake   uliojichomoza hivi karibuni wa kutoa ajira endapo Vijana hao watajituma  vilivyo. “ Nataka kuona Timu za Jimbo langu la Kitope zinashiriki na kufanya   vizuri katika mashindano ya Wilaya, Mikoa na hata Taifa. Lakini  kitachosaidia zaidi kwenu ni juhudi ya kuzingatia mazoezi  yatakayofuatiwa na nguvu za misaada ya Viongozi wenu”. Alisisitiza  Balozi Seif. 
   Akizungumzia matatizoyanayozikabili Timu hizo Balozi Seif atajaribu  kuzungumza  na wafadhili mbali mbali wa michezo ili kuona namna gani  wanaweza kusaidia uimarishaji wa uwanja wa uhakika na wa kisasa ndani ya  jimbo hilo. 
   Alisema suala hilo litakwenda sambamba na  upatikanaji wa vifaa vya  michezo ikiwemo Mipira, Nyavu Magoli na Jezi ambazo alisema zimo ndani  ya uwezo wake kulingana na utaratibu aliokwishauanzisha tokea alipoanza  kuliongoza jimbo hilo. 
   Kuhusu suala la uanzishwaji wa jengo la kudumu la Klabu Balozi Seif  aliwaagiza wanamichezo hao kuanza shughuli za maandalizi ya msingi kwa  vile tayari wameshaanza kukusanya nguvu za pamoja. Alisema katika kuunga mkono jitihada hizo za wanamichezo atahakikisha  anasaidia nguvu za unyanyuaji jengo kwa hatua ya matofali na kuangalia  mbinu za kuendeleza ujenzi huo.
    Balozi Seif Ali Iddi akiwa pia Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  aliwakumbusha wanamichezo hao kuwa  waangalifu kutokana na ushawishi  wanaoendelea kusambaziwa  wa kutaka kuingizwa katika vurugu za kisiasa  kwa kisingizio cha Kidini. Balozi Seif alitahadharisha kwamba ushawishi huo unaweza kuyayusha  kabisa amani na muda wa Vijana hao wa kushiriki kikamilifu katika  michezo yao endapo wataamua kuupokea.
    Mapema wanamichezo hao walimueleza Balozi Seif  matatizo yanayowakabili  katika katika harakati zao za kuendeleza michezo ambayo yamekuwa  yakipunguza kasi yao ya ufanisi. Wawakilishi wa wanamichezo hao Khamis Mswahili Mwinyi, Ngamia Mohd  Ngamia na Amour Amour kwa pamoja walielezea changamoto zinazowakabili  katika sekta ya michezo ikiwa ni pamoja na uhaba wa vifaa vya michezo,  ujenzi wa Jengo la Klabu pamoja na uanzishwaji wa mashindano ya kombe la  Mbunge wa Jimbo hilo ambayo tayari yamesharidhiwa na Mbunge mwenyewe  kwa kukubali kutoa Vikombe na zawadi kwa washindi.
    Walisema kufanikiwa kwa changamoto hizo kutawawezesha Vijana waliowengi  wa jimbo hilo kuwepuka kusambaratika pamoja na vishawishi vinavyoweza   kuwapelekea kujiingiza katika matendo maovu. 
   Katika kikao hicho Mbunge huyo wa Jimbo la Kitope Balozi Seif Ali Iddi  alikabidhi seti ya Jezi na Fedha Taslimu kwa Timu ya Soka ya Kitope  United  inayojiandaa na usajili kwa ajili yua mashindano yajayo. 
  Na
   Othman Khamis Ame 
  Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar