Pages

Sunday, June 17, 2012

Shein amteua Joel Thomas kuwa mjumbe wa baraza la wawakilishi

Na Juma Mohammed,
MAELEZO Zanzibar

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohammed Shein,amemteua Marina Joel Thomas kuwa Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.

Taarifa ya Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Dk. Abdulhamid Yahya Mzee,kwa vyombo vya habari imesema uteuzi huo umeanza Juni 17 mwaka huu.

Rais amefanya uteuzi huo chini ya kifungu 66 cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984.

Katiba ya Zanzibar inampa uwezo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuteuwa watu kumi kuwa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.

Walioteuliwa kupitia nafasi hizo na nyadhifa zao za sasa kwenye mabano ni Balozi Seif Ali Idd(Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar), Mohammed Aboud Mohammed(Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais) Omar Yussuf Mzee(Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Fedha Uchumi na Mipango ya Maendeleo).

Wengine ni Zainab Omar( Waziri wa Ustawi wa Jamii,Maendeleo Vijana Wanawake na Watoto), Ali Mzee Ali, Sira Mwamboya (Naibu Waziri wa Afya) Juma Duni Haji (Waziri wa Afya), Fatma Abdulhabib Ferej(Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais) Ramadhan Abdallah Shabaan( Waziri wa Ardhi, Maji na Maendeleo ya Makaazi) na Marina Joel Thomas.

Kikao cha Baraza la Wawakilishi kinatarajiwa kuendelea kesho kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kuanza kujadili bajeti ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar iliyowasilishwa Jumatano wiki hii.

Katika bajeti yake SMZ inatarajia kutumia jumla ya TZS 648.9 bilioni katika mwaka wa fedha wa 2012/13, ikiwa ni ongezeko la asilimia 38.2 kutoka shilingi 469.4 bilioni zinazotarajiwa kutumika hadi kufikia mwisho wa Juni mwaka huu.

Serikali pia inatarajia kuanza mwaka wa fedha ikiwa na bakaa ya shilingi 5.9 bilioni. Katika hotuba yake Waziri nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Fedha,Uchumi na Mipango ya Maendeleo,Omar Yussuf Mzee alisema kwa kuzingatia uwezo wa sasa wa Serikali katika mapato yake kutokana na vyanzo vya ndani, yanatarajia kufikia jumla ya shilingi 280.7 bilioni na hivyo kufanya jumla ya mapato hayo kufikia shilingi 286.6 bilioni.

Waziri huyo aliwaambiwa Wajumbe wa Baraza kwamba Fedha hizo ni mjumuisho wa mapato ya Kodi na yasiyo ya kodi, ambapo Kiasi hicho cha mapato cha shilingi 286.6 bilioni kitaacha nakisi katika Bajeti ya shilingi 362.3 bilioni.

Popular Posts