Pages

Wednesday, July 25, 2012

SERIKALI YA TANZANIA : HATUJADHULUMU MALIPO YA WAHANGA

NA MAGRETH KINABO – MAELEZO

SERIKALI imesema kuwa hakuna malipo ya kiasi kidogo cha fedha kilicholipwa kwa waathirika wa mlipuko wa mabomu ya Kambi ya jeshi ya Mbagala yaliyotokea mwaka 2009 kama ilivyoripotiwa na gazeti moja la kila wiki la hapa nchini hivi karibuni.

Akizungumza na Idara ya Habari( MAELEZO) jana ofisini kwake , Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadick alisema hakuna fidia ya Shs. 1400 na Shs. 2500 iliyotolewa kuwa ni ya uharibifu wa jumla ya fidia za malipo kwa wahanga hao, bali malipo hayo ni tofauti ya kiasi cha fedha kilichokuwa kinadaiwa na wahanga hao ambacho kilichobakia.

‘’ Unajua malipo ya wahanga hao yalifanyika katika awamu mbili. Hivyo kiasi cha fedha cha malipo hayo yaliyotolewa katika hundi hizo , ambayo iliripotiwa katika gazeti hilo ni malipo ya awamu ya tatu. Malipo hayo ni tofauti ya fedha kilichokuwa kinadaiwa na si kweli kuwa wahanga hao walilipwa fedha hizo kama jumla ya fidia za malipo yao,’’ alifafanua Mkuu huyo wa Mkoa.

Mkuu huyo wa Mkoa, aliongeza kuwa habari hiyo iliyoandikwa sio sahihi na haikufuata maadili ya uandishi wa habari kwani hakuweka wazi usahihi wa taarifa hiyo.Serikali haijamdhulumu mtu yeyote, bali inalipa kutokana malipo stahili.

‘’Ninaomba waandishi wa habari waandike habari walizozifanyika utafiti wa kina wa pande zote ilikuepusha utoaji wa taarifa zisizosahihi,’’ alisisitiza.

Aidha Mkuu huyo alisema malipo ya waathirika hao yanatolewa kwa awamu tofauti na kwa idadi ya watu maalum, kwa sababu ya kuepusha utoaji wa malipo yasiyostahili. Hivyo aliwataka waathirika hao kuvuta subira kwa kuwa malipo hayo bado yanaendelea.

Naye Mtathimini Mkuu wa malipo hayo, Victor Ndonne akizungumzia kuhusu suala hilo alisema hundi za malipo ya sh. 1000 na zilizotajwa hapo juu ni za tofauti ya kiasi cha fedha kilichobakia baada ya wahanga hao kutoridhika na malipo hayo yaliyotolewa katika awamu ya kwanza na awamu ya pili.

‘’ Fedha hizi zimelipwa baada ya kufanyika kwa tathimini mpya Agosti 18 mwaka 2011, ambapo ilioneka baadhi ya wahanga hawakurithika na fidia walizolipwa,’’ alisema Ndonne .

Alifafanua kuwa orodha ya wahanga wanaodaii malipa yao ni 2,575, hivyo hundi zilizotolewa hadi sasa ni 295 kwa ajili ya malipo hayo, ambapo hundi 244 zimeshakabidhiwa kwa wananchi husika, hundi nyingine 18 majina yamebandikwa katika eneo la Mbagala Kuu na Ofisi ya Mkurugenzi wa Wilaya ya Temeke, zaidi ya wiki moja iliyopita na wanasubiri wananchi waende kuchukua.

Ndonne alisema hundi 32 zimeonekana kuwa na matatizo mbalimbali mfano majina ya vitambulisho vyao ni tofauti na yaliyoandikwa katika hundi na majina mengine ya hundi hizo wahusika wameshafariki dunia. Aidha aliongeza kuwa hundi moja imeonekana majina yamejirudia.

Alisema kuwa hundi za malipo ya fedha ya wahanga hao zilitolewa kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha uliopita. Malipo ya fedha zingine zitatolewa mwaka huu wa fedha wa 2012/2013 mara baada ya Serikali kuidhinisha.

Popular Posts