Pages

Friday, June 8, 2012

MAONI YA OTHMAN MASOUD KUHUSU MASUALA YA MUUNGANO

4.0 HITIMISHO
4.1 Muungano wetu hautalindwa kwa siasa na kuusifu pekee na kuwaita wale wanaoukosoa kuwa ni maadui wa Muungano ingawa wapenzi wa Muungano wenyewe wanazikubali kasoro hizo hizo na hata wameziandika na kuzifanyia vikao. Muungano utalindwa kwa kuwekewa misingi madhubuti iliyo wazi na ambayo italindwa kwa misingi ya Katiba na Sheria inayokubalika na ambayo itatokana na ridhaa za washirika wa Muungano.

4.2 Mifano ipo mingi. Muungano wa Uingereza (England) na Scotland ingawa ulianzia mwaka 1603 lakini ulijadiliwa rasmi mwaka 1705 na kuanzishwa rasmi kisheria mwaka 1707. Hata hivyo miaka ya 1990 imeshuhudia ukizungumzwa tena na kuafikiwa kurejeshwa kwa Bunge la ndani la Scotland. Aidha, kwa upande mwengine, ingawa Uingereza iliungana rasmi na Ireland mwaka 1800 kwa Sheria ya “Union of Great Britan and Ireland” lakini kwa kukosekana misingi madhubuti mwaka 1922 majimbo 26 yalijitoa katika Muungano na kuanzisha Irish Free State ambayo sasa ni Ireland. Mfano mwengine, ambao pengine si mzuri ni ule wa Canada na Uingereza. Ingawa Canada ilipewa hadhi ya kuwa Dominion kupitia Sheria ya British North America Act ya 1867 lakini bado kulikuwa na matatizo mengi ambayo yalifanyiwa kazi ambako kulipelekea kutungwa Sheria ya kuweka bayana masuala yenye mzozo kwa Sheria ya Statute ya Westminster ya 1931.

4.3 Hali ni tofauti katika Muungano wa Tanzania ambapo marekebisho mengi ya kikatiba, kishera na kisera yanafanya Muungano kuwa na matatizo zaidi kwa vile kiini cha Kero za Muungano hakijashughulikiwa. Masuala ambayo hayana majibu ni mengi ndani ya Muungano.

4.4 Niliyoyaeleza ni mifano tu ya masuala hayo mengi. Kinachojidhihirisha ni kuwa tatizo sio la idadi ya Serikali tu lakini ni zaidi ya hapo. Tatizo la msingi ni lile la Kanuni za msingi za Muungano kutozingatiwa na kutopatiwa majibu. Kutokana na Kasoro hizo ndio maana Muungano wetu kama ulivyo hivi sasa hauwezi kuhimili mabadiliko ya kisiasa.

4.5 Hakuna Muungano madhubuti ambao unategemea kulindwa na sera za chama. Muungano madhubuti ni ule unaolindwa na misingi madhubuti, uwazi na wenye majibu kwa masuali yanayohusu nguzo kuu za Muungano huo.

Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar Mh Othmani Masoud.

Popular Posts